Рет қаралды 19,300
Mbiu ya Pasaka
Sasa jeshi la malaika wa Mbinguni wafurahi. Yafurahi mambo ya Mbinguni, na mbiu ya wokovu ipigwe kutangaza ushindi wa mfalme mkuu. Nayo nchi iliyoangazwa na nuru kubwa sana ifurahi na kwa kuwa imemulikwa na mwanga wa mfalme wa milele, itambue ya kuwa imeondolewa na giza la ulimwengu.
Naye Mama Kanisa aliyepambwa vizuri kwa taa nyingi zenye kuwaka afurahi na sauti za watu zivume katika ukumbi huu.
Bwana awe nanyi
Awe rohoni mwako
Inueni mioyo
Tumeiinua kwa Bwana
Tumshukuru Bwana Mungu wetu
Ni vyema na haki
Ni vyema na haki tuziimbe sifa za Mungu Baba Mwenyeziasiyeonekana, na za Mwanaye wa pekee, Bwana wetu Yesu Kristu, kwa moyo wote na akili zetu zote na kwa sauti zetu, Yeye alitulipia deni la Adamu kwa Baba wa milele, na kwa damu yake takatifu akafuta mashtaka ya ile dhambi ya kale.
Hakika hii ndio sikukuu ya Pasaka, anapochinjwa yule mwana kondoo halisi ambaye kwa damu yake milango ya waamini inabarikiwa.
Huu ndio usiku ulipowatoa Misri mara ya kwanza baba zetu, wana wa Israeli, ukawavusha pakavu katika Bahari ya Shamu.
Huu basi ndio usiku uliondoa giza la dhambi kwa nuru ya ile nguzo ya moto.
Huu ndio usiku ambapo leo popote duniani wenye kumsadiki kristu wanatengwa na maovu ya dunia na giza la dhambi, wanarudishiwa neema na kushirikishwa utakatifu.
Huu ndiyo usiku, ambapo Kristu alikata minyororo ya mauti, akatoka kuzimu ameshinda, kwa maana kuzaliwa hakungalitifaa kitu, tusingali kombolewa.
Lo, jinsi gani wema wako ni waajabu kwetu sisi!
Lo, wema gani wa upendo usiopimika wa kumtoa Mwanao upate kumkomboa mtumwa!
Lo, dhambi ya Adamu hakikaililazimika ikafutwa kwa kifu cha Kristu!
Lo, kosa lenye bahati, lililostahili kumpata Mkombozi mkuu kama Huyo!
Kwahiyo utakatifu wa usiku huu, wafukuza dhambi, wafuta makosa, huwarudishia usafi walioanguka na furaha wenye huzuni.
Basi ee Baba mwema, kwa ajili ya neema ya usiku huu upokee sadaka ya jioni ya kukusifu. Kanisa takatifu linakupa sadaka hii kwa mikono ya watumishi wake, linakutolea mshumaa huu wa nta ya nyuki.
Lo, usiku uliobarikiwa kweli, yalipounganishwa ya Mbingu na ya nchi, ya Mungu na ya mwanadamu.
Basi, ee Bwana, tunakusihi, mshumaa huu uliobarikiwa kwa heshima ya jina Lako, uendelee kuwaaka na kuondoa giza la usiku huu.
Tena uupokee kama harufu nzuri, uchanganyike na nuru za Mbinguni.
Nyota ya asubuhi iukute unawaka yaani nyota ile isiyotua kamwe, ndiye Kristu Mwanao, aliyetoka kuzimu, akawaangaza wanadamu kwa utukufu, naye anaishi na kutawala daima na milele.
W. Amina