Рет қаралды 4,480
Karismatiki Katoliki ni mwamko mmojawapo katika Kanisa Katoliki ambao unakazia suala la uwazi zaidi kwa Uwepo na Nguvu za Roho Mtakatifu na Karama zake; mabadiliko ya kiroho ya mtu binafsi na Kanisa zima kwa ujumla.
KUZALIWA KWA UPYAISHO WA KIKARISMATIKI KATOLIKI
Mara nyingi watu wananiuliza kama nilishawahi kuchoka kuhadithia kilichotokea katika Wikiendi ya Dukweni. Kamwe sijawahi kuchoka, kwa sababu ni hadithi ya kimapenzi - hadithi ya jibu la kipekee na la neema la Mungu kwa maombi ya watu fulani wa kawaida sana.
Katika kipindi cha masika cha mwaka 1966, maprofesa wawili wa chuo cha Dukweni walikuwa WAKIOMBA, WAKITAFUTA NA KUBISHA. Walikuwa wamejiahidi kuomba kila siku kwa miminiko kuu la Roho Mtakatifu katika maisha yao wakitumia Sikwensia ya Pentekoste. Katikati ya kipindi hiki cha maombi, marafiki zao kadhaa waliwapa vitabu viwili: Msalaba na Upanga (The Cross and the Switchblade) na Wananena kwa Lugha Nyingine (They Speak With Other Tongues). Vitabu vyote vinaelezea uzoefu wa Ubatizo katika Roho Mtakatifu. Hawa maprofesa wakatambua kuwa Ubatizo katika Roho Mtakatifu ndio hasa waliokuwa wakiutafuta.
Januari 1967, Wakatoliki wanne kutoka Dukweni walihudhuria kwa mara ya kwanza mkutano wa sala wa Kikarismatiki wa mchanganyiko wa madhehebu - mkutano wa Chapel Hill - nyumbani kwa bi Flo Dodge, Mpresbiteri aliyejazwa Roho Mtakatifu. Jambo la kuvutia zaidi, miezi michache kabla Wakatoliki hawa hawajaja, Bwana Alimuongoza bi Flo kusoma Isaya 48 ambapo Anatangaza kwamba Yu karibu kutenda ‘jambo jipya’. Kwa hakika, Mungu Alikuwa Yu karibu kutenda jambo jipya miongoni mwa Wakatoliki kama matokeo ya mkutano wa sala. Wale watu kutoka Dukweni walivutiwa na kile walichokishuhudia kule. Tarehe 20 Januari, wawili miongoni mwao wakarudi tena. Wakapokea Ubatizo katika Roho Mtakatifu na kuanza kudhihirisha vipawa vya kikarismatiki. Wakarudi nyumbani kuomba na wale wengine wawili ambao hawakuhudhuria usiku ule.
Kipindi hiki nilikuwa ni mwanachama wa kikundi cha kusoma Maandiko cha Chi Rho kilichokuwa kikikutana pale chuoni Dukweni. Wawili kati ya hawa maprofesa walikuwa ni wasimamizi wa kikundi hiki, na ingawa hawakutuambia moja kwa moja juu ya uzoefu wao wa Kikarismatiki, wale waliowajua vizuri walitambua wana mwako wa furaha mpya. Tulikuwa tunapanga mafungo yetu ya Februari na maprofesa wakapendekeza mada mpya: “Roho Mtakatifu.” Katika maandalizi kwa ajili ya mafungo, walituambia tuombe kwa mategemeo/matarajio, tusome kitabu cha Msalaba na Upanga, na tusome sura nne za kwanza za kitabu cha Matendo ya Mitume.
VENI CREATOR SPIRITUS, “NJOO ROHO MUUMBAJI”
Siku chache kabla ya mafungo, nilipiga magoti chumbani kwangu na kuomba,”Bwana, naamini nimekwisha kumpokea Roho Wako katika Ubatizo na Kipaimara. Lakini kama inawezekana kwa Roho Wako kutenda kazi zaidi maishani mwangu kuliko ambavyo amekuwa hadi sasa, NAMHITAJI!” Jibu kuu na la ajabu la maombi yangu lilikuwa li karibu kuja.
Tarehe 17 Februari watu 25 tuliondoka chuoni kwenda katika nyumba ya mafungo ya The Ark and The Dove (Safina na Njiwa) iliyokuwa nje kidogo ya jiji. Tulipokuwa tukikusanyika katika kila kipindi, maprofesa wetu walituambia tuimbe kama maombi tenzi ya zamani Veni Creator Spiritus, “Njoo Roho Muumbaji”. Ijumaa usiku kulikuwa na tafakari kwa Mama Maria. Kisha tukawa na Huduma ya Kitubio. Katika Injili ya Yohana tulisoma kwamba Roho Mtakatifu Atakapokuja Ataushuhudia Ulimwengu kwa habari ya dhambi. Hicho ndicho kilichotokea miongoni mwetu wakati tukitubu katika Sakramenti ya Upatanisho.
Jumamosi mshiriki mmoja wa kikundi cha sala cha Chapel Hill alikuja kuzungumza juu ya Matendo ya Mitume sura ya pili. Tulichoambiwa ni kwamba alikuwa ni rafiki wa Kiprotestanti wa maprofesa wetu. Ingawa uwasilishaji wake ulikuwa ni rahisi, ulijawa na nguvu za kiroho. Alizungumzia kujisalimisha kwa Yesu kama Bwana na Mkuu. Alimwelezea Roho Mtakatifu kama Nafsi Anayemtia nguvu kila siku. Huyu alikuwa mtu ambaye kwa hakika alionekana kumjua Yesu kwa undani na binafsi! Alijua nguvu za Roho Mtakatifu kama Mitume walivyojua. Nilijua nilitaka kile ambacho mtu huyu alikuwa nacho na niliandika katika notisi zangu, “Yesu, Uwe halisi kwangu.”
Katika majadiliano baada ya mafundisho yake, David Mangan akapendekeza kwamba tufunge mafungo yetu kwa kupyaisha Kipaimara chetu…kwamba sisi, kama vijana wakubwa, tuseme ‘ndiyo’ binafsi kwa Roho Mtakatifu. Niliunganisha mkono wangu na wake na kusema, “hata kama hakuna mwingine anayetaka kufanya hivi, ninafanya.” Kisha nilichana karatasi na kuandika, “Nataka muujiza!”, na kuibandika katika ubao wa matangazo.
SOMA ZAIDI
www.jamiiforums.com/threads/n...